UMEPATA kusikia jina la Dk. Asanterabi Malima?
Jambo moja ambalo wanafunzi waliosoma naye nchini Tanzania
hawabishani kuhusu Malima ni ukweli kwamba alikuwa ni mwanafunzi mwenye
akili nyingi darasani.
Shafii Dauda ambaye alikuwa mwanafunzi wa kidato cha kwanza katika
Shule ya Sekondari Azania jijini Dar es Salaam, anamkumbuka Asanterabi
kama mwanafunzi mwenye akili aliyefanya vizuri sana katika masomo yake
ya kumaliza kidato cha nne.
Shafii, ambaye sasa ni miongoni mwa watangazaji na wachambuzi
maarufu wa mchezo wa soka hapa nchini alikuwa kidato cha kwanza wakati
Malima alikuwa kidato cha nne.
Akili ile ya Malima imemfikisha nchini Marekani ambako sasa amefanya
ugunduzi wa kidude chenye saizi ya pini ndogo (milimita 0.250)
kinachoweza kubaini magonjwa ya kuambukiza, kansa na moyo katika hatua
ya awali kabisa.
Ugunduzi huu, utakapofika mwisho wake, unaweza kuokoa maisha ya watu
wengi duniani. Fikiria tu kwamba unakuwa na kifaa ambacho mojawapo ya
magonjwa hayo yakikuanza unaubaini mapema na kwenda kutibiwa.
Mamilioni ya watu wataokolewa maisha yao na kijana huyu wa Kitanzania.
“Siku zote nimekuwa na ndoto za kugundua kitu ambacho kitaweza
kuokoa maisha ya watu. Baba yangu alifariki kwa ugonjwa wa moyo ambao
ungegundulika mapema kama kungekuwa na kifaa kama hiki.
“Kwa sasa sitaweza kuokoa maisha ya baba yangu lakini ninaweza kuokoa
maisha ya wazazi au watoto wa watu wengine kutokana na ugunduzi huu
nilioufanya. Nafurahi kwamba ndoto yangu imetimia.
“Kansa, baadhi ya magonjwa ya kuambukizwa na magonjwa ya moyo huwa
yanachelewa sana kugundulika. Watu wengi hupoteza maisha, na kwa nchi
zilizoendelea hutumia pesa nyingi sana kuwatibu waathirika.
“Kifaa nilichogundua ni kidude cha ukubwa wa pini (0.250mm)
kinachoweza kupima na kugundua hayo magonjwa mapema. Ili, yaweze
kutibika kirahisi, kuokoa maisha na kupunguza gharama,” anasema
Asanterabi katika mazungumzo yake na Raia Mwema yaliyofanyika kwa njia ya mtandao juzi Jumatatu.
Asanterabi ni mtoto wa aliyepata kuwa waziri wa fedha wa Tanzania,
Profesa Kighoma Ali Malima, aliyefariki dunia Agosti 6, 1995 jijini
London, Uingereza, katika mojawapo ya vifo vya kushtusha katika
historia ya Tanzania.
Kifaa alichokigundia kijana huyu wa Kitanzania kinafahamika kwa jina la Biolom na
ugunduzi huu aliufanya akishirikiana na wanafunzi wenzake wawili wa
Chuo Kikuu cha Northeastern kilichopo Boston; Cihan Yilmaz na Jaydev
Upponi.
Pamoja na udogo wake, kipini hicho kina jumla ya maeneo manne –yote
yenye kazi maalumu, na ubunifu huo tayari umetambuliwa na Serikali ya
Marekani.
Katika mazungumzo yake na vyombo vya habari vya Marekani, Asanterabi
alipata kusema kwamba vifaa vingi vya kisasa hubaini magonjwa; kwa
mfano kansa, katika wakati ambapo ni vigumu mtu kupata tiba na kupona.
“Kazi yetu hii itakapokamilika, tutaweza kubaini magonjwa haraka
zaidi na mapema zaidi na hivyo watu watapata tiba mapema na kuokoa
maisha.
“Nchini kwangu (Tanzania), akinamama wengi hufariki dunia kwa sababu
ya kuugua ugonjwa wa kansa ya kizazi, kifaa hiki kitaweza kusaidia watu
wengi kupona kutoka katika matatizo yao,” alisema.
Kidude hicho ni kidogo sana kwa umbo na namuuliza kama wameamua
iwapo mtu anaweza kukinunua na kubaki nacho nyumbani akijitazama
mwenyewe au ni lazima aende hospitali.
“Dhamira yetu hapo ni kipimo kitumike mtu akienda hospitali au kliniki (for annual check-up). Lakini japokuwa kinafanya kazi, kupata ruhusa kwa kukiingiza kama pini ni vigumu. Tunafanya vipimo (test) kwa kupima damu iliyotoka kwa mgonjwa,” anasema.
Asanterabi ni zao la mfumo wa masomo wa kawaida uliokuwepo hapa
nchini miaka michache iliyopita (kabla ya ujio wa hizi za kata na ‘academy’).
Alisoma katika Shule ya Sekondari ya Tambaza jijini Dar es Salaam kwa mwaka mmoja kabla ya kuhamia Azania.
Miaka 20 iliyopita, hizi zilikuwa ni shule zilizokuwa zikichukua
watoto waliofaulu vizuri kimasomo miongoni mwa wanafunzi wa shule za
msingi za Mkoa wa Dar es Salaam.
“Tambaza nilisoma mwaka mmoja tu lakini kutokana na fujo zilizokuwapo
nikahamishwa na wazazi na ndipo nikaenda Azania nilikosoma mpaka
kumaliza kidato cha nne. Nashukuru kwamba nilifaulu vizuri kwa kupata
daraja la kwanza. Kimsingi, nilipata alama A katika masomo yangu yote,”
anasema.
Pamoja na muda wote alioutumia Marekani na umaarufu ambao ameupata
kama mmoja wa vijana wenye bongo zinazochemka nchini humo, Asanterabi
bado hajasahau maisha ya hapa nchini na, hususan, maisha ya shule.
Kimsingi, Asanterabi anasikitishwa sana na matokeo mabovu ambayo
baadhi ya shule alizosoma katika miaka ya nyuma zimekuwa zikiyapata
katika miaka ya karibuni.
“Kwa kweli nakumbuka sana walimu wangu. Pale Tambaza, kwa mfano,
namkumbuka sana mwalimu mmoja alikuwa anaitwa Mama Msuya, huyu nadhani
ndiye alikuwa mwalimu bora kuliko wote pale. Huyu alikuwa anafundisha
Jiografia.
“Katika shule ya Azania, namkumbuka sana Mama Shija ambaye naye
alikuwa akitufundisha somo la Kemia. Mzizima namkumbuka sana mwalimu
mmoja alikuwa anaitwa Thind - best mathematician ever (mwana hisabati
bora kuliko wote niliowahi kufundishwa nao).
“Elimu ni sehemu nyingine ambao inanisisimua mno. Nimefuatilia
katika tovuti ya Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi ( moe.org.tz )
kuwa mwaka 2011, karibu asilimia 50 ya wanafunzi walipata alama sifuri.
Tambaza, Forodhani, Kibasila na Azania zilikuwa na watu wenye akili
kuliko wote, pengine Tanzania nzima.
“Niko sasa nafanya kazi na vichwa vya bongo huku Marekani tuone
tunaweza kufanya nini kutoa mchango kwa "online video learning"
(mafunzo kwa njia ya mtandao maana wengi wetu tulisoma bure tu na huo
utakuwa sehemu ya mchango wetu kwa Taifa,” anasema.
Kutokana na ubunifu huo alioufanya na wenzake hao, Malima sasa
anatakiwa kuanzisha kampuni ambayo itafanya biashara ya ubunifu huo
utakaoleta mapinduzi katika sekta ya afya duniani kote.
Haya ni mabadiliko makubwa katika maisha ya Asanterabi ambaye
aliwahi kunukuliwa na vyombo vya habari vya Marekani akisema kwamba
siasa iko kwenye damu ya familia yao.
Baba yake alikuwa mwanasiasa na msomi maarufu nchini na kaka wa
Asanterabi, Adam, sasa ni Naibu Waziri wa Fedha katika serikali ya Rais
Jakaya Kikwete. Pia ndiye Mbunge wa Jimbo la Mkuranga kupitia Chama
Cha Mapinduzi (CCM).
“Kusema kweli mimi sijawahi kujiona kama mjasiriamali
(mfanyabiashara). Watu wengi walijua kwamba nitakapokuwa mkubwa
nitafuata tu nyayo za wazee wangu. Lakini leo niko hapa.
“Kwenye maisha yangu, sikutaraji kwamba ipo siku nitakuja kufanya
ubunifu kama huu. Baada ya kufika hapa nilipofika, sasa naamini kwamba
naweza kupiga hatua zaidi,” anasema.
Ingawa fedha si msukumo mkubwa katika maisha ya Asanterabi, ugunduzi
huu unaweza kumfanya kuwa mmoja wa Watanzania matajiri endapo kidude
hiki kitaanza kuuzwa.
Hesabu zake ziko hivi.
“Tunafikiri kitakapokuwa tayari, kidude kimoja kinaweza kuuzwa kwa
wastani wa dola moja hivi ya Marekani (Shilingi 1650) kama tukiweza
kufanya uzalishaji mkubwa.
“Gharama ya kupimwa inaweza kugharimu kiasi cha kati ya dola 10-15.
Mahospitali huwa wanachaji hela nyingi mno kama daktari ndio atafanya
vipimo na maamuzi. Ila kama ni nesi gharama si kubwa,” anasema.
Katika dunia yenye watu zaidi ya bilioni sita, uwezekano wa kuuza
pini hizo milioni mia moja kwa mwaka ni mkubwa na kwa kiasi hicho
pekee, mauzo ya zaidi ya dola milioni 100 kwa mwaka (zaidi ya shilingi
bilioni 165) yanawezekana.
Asanterabi na wenzake watakuwa na mgawo wao hapo na ifahamike kwa
sababu ya sheria kali za hatimiliki nchini Marekani, hizi ni fedha
ambazo familia ya wagunduzi watakula hadi kwa wajukuu, vitukuu na
kuendelea.
Safari ya Asanterabi kutoka Tanzania kwenda Marekani haikuwa rahisa
namna hiyo. Ikumbukwe kwamba alifiwa na baba yake wakati ndiyo kwanza
akiwa na umri wa miaka 15 tu.
Ni msiba ambao nusura ubadili kabisa maisha ya kijana huyu ambaye
baadhi ya wanafunzi waliowahi kusoma naye wanamtambua kwa jina la
“Mzaramo wa Chole.”
Chole ni miongoni mwa mitaa maarufu ya eneo la Oysterbay jijini Dar
es Salaam ambako Asanterabi alikulia. Pengine, jina hilo linatokana na
ukweli kwamba kuna watu wachache wa kabila la Wazaramo analotoka Malima
wanaoishi huko.
Majina ya namna hii hayakuwa na maana ya ubaguzi wa kikabila lakini
ni sehemu ya utani wa kikabila uliokuwa Tanzania wakati huu.
Utafiti na ubunifu huu wa Asanterabi si habari kubwa hapa Tanzania
pekee kwani inaonekana kwamba hata Marekani nako ameanza kutambulika.
Juni mwaka huu, wakati wa sherehe za maadhimisho ya Wiki ya Afrika
katika Jimbo la Massachussets uliko mji wa Boston, Gavana wa Jimbo
hilo, Deval Patrick, alimpa Asanterabi tuzo maalumu ya Ujasiriamali
akimpongeza kwa ubunifu wake huo utakaosababisha nafuu kwa maisha ya
wanadamu na pia ukuaji wa uchumi wa eneo hilo.
“Si kwamba ugunduzi huu utabadili maisha ya wengi na uchumi kwa
wakazi wa Marekani pekee, lakini ugunduzi huu utasaidia sana kuokoa
maisha ya mamilioni ya wananchi katika nchi anakotoka Malima ya
Tanzania,” alisema Gavana huyo.
Miaka michache iliyopita, Asanterabi alikuwa akijipanga kuwa mmoja
wa waajiriwa katika mojawapo ya kampuni kubwa duniani ya Toshiba,
lakini sasa ugunduzi huu umemfanya kujiandaa kuwa mmoja wa viongozi wa
kampuni muhimu hapa duniani.
Pamoja na umbali mkubwa uliopo sasa, baadhi ya watu wanaomfahamu
Asanterabi wanamkumbuka kama kijana mpole ambaye hakuharibiwa na ukubwa
wa jina la baba yake.
“Mzaramo wa Chole alikuwa mpole sana kipindi kile anasoma Azania na
kwa kweli hakuwa na mambo mengi kama walivyo watoto wengi wa wakubwa,”
anasema Mintanga Malulu aliyesoma katika shule hiyo wakati mmoja na
Asanterabi.
Jambo zuri kuhusu Asanterabi ni kwamba ni mzalendo na anayependa nchi yake. Katika mazungumzo yake na Raia Mwema, alisema kwamba kwa namna yoyote ile ugunduzi wake huo utaifaidisha Tanzania.
Tayari Tume ya Sayansi na Teknolojia Tanzania (Costech) imetangaza
kuvutiwa na mafanikio ya Asanterabi katika Nyanja hiyo ya sayansi.
Taarifa iliyotolewa na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi hiyo, Dk.
Flora Tibazarwa, inasema ingawa utafiti huo bado haujafikia katika
hatua ya mwisho, matumaini ni makubwa.
“Tuna taarifa kuhusu ugunduzi wa Dk. Malima lakini hatuwezi kusema
chochote kwa sasa kwa vile bado uko katika hatua za awali na haujapita
katika vipimo vyote. Jambo zuri ni kwamba dalili za kufanikiwa ni
kubwa,” ilisema taarifa hiyo.
Ni safari ndefu, ndefu sana kutoka Tanzania hadi Marekani. Lakini,
kama mwisho wake ni kama ule wa Asanterabi, safari inakuwa njema.
Wakati tukiagana baada ya kumaliza mazungumzo yetu, bado alionyesha
kusikitishwa na matokeo katika shule za sekondari maarufu; Hivi, kuna
nini kinatokea huko kwa Azania na Tambaza?
Sikuwa na majibu. Labda nitapata kama nitafanya utafiti. Labda,
itabidi Asanterabi agundue kidude kingine kitakachotoa majibu kuhusu
kushuka kwa elimu hapa nchini.
Swali moja kubwa ambalo nimejiuliza baada ya mazungumzo yangu na
Asanterabi ni moja tu; Hivi kweli Taifa hili litakuja kutoa akina
Asanterabi wengine katika miaka 20 ijayo katika mfumo wetu wa elimu
tulionao sasa?